Mahakama kusikiliza hoja uvamizi wa Israel Palestina

0
164

Mahakama Kuu ya Umoja wa Mataifa leo Jumatatu inafungua wiki ya vikao kusikiliza hoja za kisheria kuhusu madai ya Israel kuyakalia kwa mabavu maeneo ya Wapalestina, huku zaidi ya majimbo 50 yakitarajiwa kutoa hoja zao kwa majaji.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Palestina, Riyad al-Maliki atazungumza kwanza katika mashauri ya kisheria katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ), mjini The Hague.

Mwaka wa 2022, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliiomba mahakama kutoa ushauri wa kisheria kuhusu madai hayo.

Wakati Israel ilipuuza suala hilo siku za nyuma, shinikizo la kisiasa limekuwa kubwa kutaka tafsiri za kisheria na hasa kutokana na vita vinavyoendelea katika Ukanda wa Gaza, ambavyo vimeua takriban Wapalestina 29,000, tangu vilipoanza kurindima Oktoba 7 mwaka jana, kulingana na maafisa wa afya wa Gaza.

Miongoni mwa nchi zilizopangwa kushiriki katika vikao hivyo ni pamoja na Marekani ambayo ni muungaji mkono mkubwa wa Israel. Nchi nyingine ni China, Urusi, Afrika Kusini na Misri. Israeli haitashiriki, ingawa imetuma mtazamo wake kwa maandishi.

Vikao hivyo ni sehemu ya msukumo wa Wapalestina kutaka taasisi za kisheria za kimataifa kuchunguza mwenendo wa Israel, ambapo haja hiyo umeongezeka zaidi tangu shambulio la Oktoba 7 lililofanywa na Hamas nchini Israel, ambalo lilisababisha vifo vya watu 1,200 na kusababisha jeshi la Israel kujibu mapigo yanayoendelea hadi sasa.

Pia vikao hivyo vya kujadili hoja za kisheria vinakuja huku kukiwa na wasiwasi unaoongezeka kuhusu mashambulizi ya ardhini yanayofanywa na Israel dhidi ya mji wa Rafah ambao ulikuwa kimbilio la mwisho la Wapalestina zaidi ya milioni moja wakitokea eneo la kusini mwa Ukanda wa Gaza ili kuepuka mashambulizi ya Israel.