Taifa la Argentina Kombe la Dunia 2022

0
276

Taifa la Argentina linakwenda kwenye fainali za mwaka huu za Kombe la dunia huko Qatar  likiwa  kwenye mikono ya moja ya nyota wakubwa  ulimwenguni  na mshindi mara saba wa tuzo ya mchezaji bora duniani ya Ballon d’or  na huyo si mwingine anaitwa Lionel Messi ametamba na kikosi cha Barcelona kabla ya kutimkia PSG ya Ufaransa.


Messi ni nani? Alizaliwa Juni 24 mwaka 1987 huko kwenye mji  wa Rosario nchini Argentina.


Nyota huyo mwenye kipaji kikubwa cha kusakata kabumbu alianza kuichezea timu ya taifa ya Argentina mwaka 2005 akiwa na miaka 18 na alikuwapo kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Argentina kilichoshiriki fainali za kombe la dunia mwaka 2006 huko nchini Ujerumani.


 Mwaka huo  Messi alimuingiza matatani aliyekuwa kocha wa timu ya taifa ya Argentina,  Jose Perekman baada ya kutomjumuisha Messi kwenye mchezo wa robo fainali ya kombe la dunia dhidi ya Ujerumani  ambapo timu ya Argentina ilifungwa, baada ya kurejea nyumbani mashabiki wengi wa soka nchini humo walicharuka juu ya mamuzi ya kocha huyo wakiamini Messi alikuwa na uwezo wa kuwavusha.


Mwaka 2010 Messi alikuwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Argentina huko Afrika Kusini kwenye fainali za kombe la dunia ambapo nyota huyo alikuwa na mchango mkubwa kwenye michuano hiyo chini ya kocha Diego Maradona ambaye sasa ni marehemu. Hata hivyo mwaka huo Messi alikumbana na ukosoaji mkali baada ya timu yake kutupwa nje kwenye hatua ya robo fainali ya kombe la dunia mashabiki wa timu hiyo walimshutumu kuwa anacheza chini ya kiwango na anaijali zaidi klabu yake ya Barcelona kuliko timu ya taifa.


Unajua kwanini watu wa Argentina walikasirika? Ipo hivi msimu wa mwaka 2010/2011 Messi alifunga jumla ya mabao 53 akiwa na Barcelona lakini hakuwa amefunga bao lolote kwenye michezo rasmi ya timu ya taifa tangu march 2009.


Mwaka 2014 yaweza kuwa ni moja ya mwaka wa kukumbwa mno kwa Lionel Messi kwenye kombe la Dunia baada ya kupoteza kwenye fainali dhidi ya Ujerumani baada ya kupambana vilivyo ila bahati ikamkata.
June 26 mwaka 2016  Lionel Messi alitangaza kustaafu kuichezea timu ya taifa ya Argentina kufuatia kupoteza kwenye fainali ya Copa America dhidi ya Chile ambayo hiyo ilikuwa ni fainali yake ya tatu kupoteza.


Mwaka 2018 Messi alishiriki fainali za kombe la dunia kwa mara ya nne na alifunga bao kwenye mchezo wa mwisho wa makundi dhidi ya Nigeria na kuwa Muargentina watatu kufunga kwenye fainali tatu tofauti za kombe la dunia akiwafikia Diego Maradona na Gabriel Batistuta.


 Mwaka 2021 Messi alishinda taji lake la kwanza kubwa akiwa na timu ya taifa baada ya kuifunga Brazil kwenye fainali ya Copa America na  kuipa timu yake taji la kwanza atangu mwaka 1993.


Muargentina huyo ndiye mfungaji bora wa muda wote wa timu ya taifa akiwa amefunga mabao 90 kwenye michezo 164 aliyoichezea timu hiyo na fainali za kombe la dunia za mwaka huu zitakuwa za mwisho kwa Messi kuichezea timu ya taifa ya Argentina. 


Messi anakwenda kushiriki fainali zake za tano za kombe la dunia mwaka huu na atakuwa nahodha wa Argentina kwenye michuano hii kubwa ambayo ndio taji pekee watu wa soka wanalomdai kwenye hii dunia.


Kaa tayari kutazama na kusikiliza Fainali za Kombe la Dunia kupitia TBC buuree kuanzia Novemba 20 – Disemba 18.