Mwakinyo aibukia Dodoma kutoka Uingereza

0
206

Baada ya kukaa nje ya ulingo kwa muda mrefu, Aprili 22 mwaka huu bondia Hassan Mwakinyo atapanda ulingoni katika uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma kukipiga dhidi ya bondia kutoka Afrika Kusini.

Mara ya mwisho Mwakinyo alipanda ulingoni Septemba 3 mwaka 2022 ambapo alipambana na bondia Liam Smith jijini Liverpool, Uingereza na kupoteza kwa TKO katika mzunguko wa nne.

Akizungumzia pambano hilo, Mwakinyo amesema “sasa narejea kwa nguvu zote na kufuta mawazo yote hasi dhidi yangu,” amesisitiza kuwa pambano hilo halilengi kumfurahisha mtu bali kukuza kipaji chake.

Hilo litakuwa pambano lake la kwanza mkoani Dodoma ambapo ametumia nafasi hiyo kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake kuendeleza mchezo huo na kuleta hamasa kubwa.