GSM kusimamia mabadiliko ya uendeshaji ndani ya Yanga

0
391

Uongozi wa Yanga umesema kuwa mchakato mzima wa kuelekea kwenye mfumo wa mabadiliko ya timu hiyo asilimia 100 unasimamiwa na Kampuni ya GSM ambao ni wadhamini wa Yanga na mpaka hatua ambayo wamefika kwa sasa ni kubwa.

Hivi karibuni Mkurugenzi wa Uwekezaji kutoka GSM Injinia Hersi Said na Alvaro Paya mwakilishi wa La Liga walikwea pipa kuelekea Hispania kwa ajili ya kukabidhiwa rasmi rasimu ya awali ya uendeshwaji wa klabu.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es salaam, Mwenyekiti wa Yanga, Dkt. Mshindo Msola amesema kuwa kuna karatasi 400 ambazo zimezungumza kuhusu mchakato huo ambao utaleta mabadiliko ndani ya Yanga kwa kufuata sheria za Serikali

Msola ameongeza kuwa walipaswa kufanya mkutano hivi karibuni ila walighairi kwa ajili ya mchakato huo ambapo leo makabidhiano ya rasimu hiyo yamefanyika huku uongozi ukiwa umeanza kuandaa mpango kazi kwa ajili ya mkutano mkuu utakaoitishwa hivi karibuni.

Mshauri kwenye masuala ya mabadiliko, Senzo Mbatha amesema kuwa anaamini kwamba kila kitu kitakuwa sawa na watafikia malengo ambayo wanayahitaji.