TBC yapanda miti Shule ya Msingi Vikunge, Kibaha

0
193

Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kwa kushirikiana na Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) na Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani wamepanda miti zaidi ya 400 katika Shule ya Msingi Vikuge iliyopo Kata ya Songe.

Miti hiyo ya matunda, kivuli na mbao imepandwa ikiwa ni utekelezaji wa kampeni ya 27 ya Kijani inayoratibiwa na TBC, yenye lengo la kupanda miti katika maeneo mbalimbali nchini ili kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Akiongoza zoezi hilo, Katibu Tawala Wilaya ya Kibaha, Moses Magogwa ameitaka jamii kulichukulia zoezi la upandaji miti kuwa sehemu ya desturi kwa kuwa lina manufaa mengi.

Katika hatua nyingine ameishukuru na kuipongeza TBC kwa kuendesha zoezi hilo na kuwa wataendelea kupanda miti kuunga mkono kampeni hiyo.

Kampeni ya 27 ya Kijani inaendeshwa na TBC kwa kufuatilia na kuhamasisha upandaji miti katika maeneo mbalimbali nchini tarehe 27 ya kila mwezi, ikiwa ni zawadi kwa Rais wa Tanzania Samia Suluhu ikiwa ni tarehe yake ya kuzaliwa.