Mkandarasi barabara ya Mikumi-Ifakara akalia kuti kavu

0
223

Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa ametoa miezi miwili kwa Mkandarasi wa Kampuni ya M/S Reynolds Construction Company kukamilisha ujenzi wa Barabara ya Mikumi-Kidatu-Ifakara, sehemu ya Kidatu-Ifakara ( Km 66.9) kwa kiwango cha lami pamoja na ujenzi wa daraja la Mto Ruaha Mkuu.

Waziri Bashungwa ametoa maagizo hayo leo wilayani Kilombero mkoani Morogoro mara baada ya kukagua barabara hiyo na daraja la Mto Ruaha Mkuu na kutoridhishwa na kasi ya ujenzi. Mkandarasi yupo nje ya muda wa mkataba wa kukamilisha mradi huo.

Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Alinanuswe Kyamba, amesema barabara hiyo na daraja la Mto Ruaha Mkuu ni sehemu ya mkakati wa Taifa kusaidia wakulima wadogo kupitia Programu ya Uendelezaji Kilimo katika Ukanda wa Kusini mwa Tanzania (SAGCOT), walioko katika Bonde la Mto Kilombero ili kuyafikia masoko ya uhakika ya mazao yao kipindi chote cha mwaka.

Mbunge wa Kilombero, Abubakar Asenga na Mbunge wa Mikumi, Denis Londo wamesema daraja hilo linasubiriwa sana na wananchi hao kwani kukamilika kwake kutafungua fursa kwa wakazi wa Kilombero na mkoa kwa ujumla.