Maafisa utamaduni na michezo wakutana

0
5743

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameziagiza halmashauri zote nchini kuthamini mchango wa kazi za maafisa utamaduni na michezo kwa kuwapangia kazi zinazoendana na taaluma yao.
 
Waziri Mkuu Majaliwa ametoa agizo hilo jijini Dodoma, wakati akifungua kikao kazi cha maafisa utamaduni na michezo.

Amesema kuna baadhi ya halmashauri nchini zinawapangia maafisa utamaduni na michezo majukumu tofauti na kazi zao, hivyo ziache mtindo huo mara moja.

Aidha, Waziri Mkuu Majaliwa ameagiza kufanyika kwa vikao hivyo zaidi ya mara moja kwa mwaka, ili kutathmini kazi zinazofanyika, kwani sekta ya utamaduni na michezo imekuwa na umuhimu kwa maendeleo ya Taifa.

Kwa upande wake Waziri Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohamed Mchengerwa amesema, wizara yake imekuwa na mchango mkubwa katika kuongeza fursa za ajira na kukuza pato la Taifa.
 
Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2003, kikao kazi cha maafisa utamaduni na michezo hufanyika kila mwaka kikiwa na lengo la kujadili, kutathmini na kupendekeza namna bora ya kuendesha sekta hiyo kwa maslahi ya  Taifa.