Wajiolojia waanika changamoto ya usahihi wa tafiti “Hatulalamiki ni udanganyifu na makusudi”

0
2505

Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Wajiolojia Tanzania Dkt. Elisante Mshiu amesema, changamoto kubwa inayoikabili tasnia hiyo ni udanganyifu katika matokeo ya tafiti.

Dkt. Mshiu ameyasema hayo mkoani Arusha wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa mwaka wa chama cha Wajiolojia Tanzania (TGS2022), ambapo mgeni rasmi alikuwa waziri wa Madini Doto Biteko.

“Kwa bahati mbaya mara nyingi kuna watafiti ambao kwa makusudi wanatoa matokeo ya tafiti ambazo sio sahihi.” amesema Dkt. Mshiu

Amesema sababu ya udanganyifu huo
ni kutokuwepo kwa kiasi sahihi cha fedha zinazotegemewa kwenye miradi na kukwepa kodi, hivyo kuikosesha serikali mapato.

Pia Dkt. Mshiu amesema wakati mwingine makosa katika tafiti yanatokana na uvivu na uzembe wa watafiti na changamoto ya uwezo wa wanafunzi wapya kufanya utafiti kutokana na kujifunza zaidi kwa nadharia.

Kutokana na changamoto hiyo, chama cha Wajiolojia kimependekeza kuanzishwa kwa mfumo wa uhakiki wa taarifa zinazotolewa na wataalam hasa za miradi ya uzalishaji, ili kuhakikisha zinakuwa sahihi.

Chama hicho pia kimependekeza serikali kuanzisha Bodi ya Usajili ya Wanajiosayansi (Geoscientist Registration Board).