Mtuambie wenzetu wamefanya uchawi gani

0
163

Rais Samia Suluhu Hassan amesema kati ya miaka 1960 – 1970 nchi ya Tanzania na nchi za Bara la Asia zilikuwa na uchumi unaolingana, ila hivi sasa nchi hizo zinaonekana kupishana kwa hatua kubwa sana.

Akizungumza Ikulu Chamwino mkoani Dodoma wakati wa hafla ya kuwaapisha Mabalozi aliowateua hivi karibuni Rais Samia amesema kwa sasa nchi za Bara la Asia zimeipita nchi ya Tanzania kwa hatua kubwa sana, jambo ambalo angependa kufahamu kuna siri gani katika hilo.

“Kwa miaka hiyo Thailand ilikuwa na DGP per Capital ya dola 166 na Tanzania tulikuwa 165, leo Thailand wapo dola 7495 na sisi tupo 1227, kwa hiyo wao wanaokwenda upande huo mtuambie wenzetu wamefanya uchawi gani kwenda haraka hivyo na sisi tunakosa nini.” Amesema Rais Samia

Aidha, Rais Samia amesema ni kweli kuwa nchi zingine wamepiga hatua kubwa ila kwa kuangalia baadhi ya rasilimali kama madini, ardhi yenye rutuba na ukanda wa bahari na maziwa Tanzania imezidi nchi hizo lakini bado katika ukuaji wa uchumi Tanzania inashindwa na nchi zingine.

Hivyo Rais Samia ametaka Diplomasia ya uchumi kufanya kazi katika eneo hilo na kutoa ushauri.