Bajeti ya serikali 2022/2023 hadharani leo

0
178

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Mwigulu Nchemba leo anawasilisha bajeti kuu ya serikali kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023.

Katika mwaka wa fedha wa 2022/2023, serikali inatarajia kutumia shilingi trilioni 41 sawa na ongezeko la asilimia 8.1 ya bajeti inayomalizika ya mwaka wa fedha wa 2021/2022.

Bajeti ya serikali iliyoidhinishwa na bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mwaka wa fedha wa 2021/2022 ilikuwa shilingi trilioni 37.9 ambapo kati ya fedha hizo shilingi trilioni 23 zilitengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi trilioni 14.9 zilikuwa ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.

Katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha baadhi ya mambo yaliyozingatiwa ni ongezeko la mishahara, ajira mpya, upandishaji wa madaraja kwa watumishi wa umma na sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika mwezi Agosti 23 mwaka huu.

Bajeti kuu ya serikali ya Tanzania kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023 inawasilishwa siku moja na bajeti za serikali za baadhi ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.