Facebook yakubali shutuma za Umoja wa Mataifa

0
1849

Mtandao wa kijamii wa Facebook umekubali shutuma zilitolewa na Umoja wa Mataifa kuwa mtandao huo ulishindwa kuzuia mazingira yaliyosaidia kuchochea ghasia nchini Myanmar.

Taarifa iliyotolewa na mtandao huo imesema kuwa habari zilizokua zikichapishwa na kusambazwa na raia wa Myanmar kupitia Facebook zilikua zikiunga mkono ukiukwaji wa haki za binadamu na hatimaye kuzusha ghasia.

Facebook imetoa taarifa hiyo kufuatia kuenea kwa ghasia nchini Myanmar dhidi ya kabila la Rohingya linaloonekana kama ni la wahamiaji nchini humo, ghasia zilizosababisha mauaji ya watu wengi.

Wakati ukitoa shutuma hizo, Umoja wa Mataifa uliitaka Facebook kufanya jitihada za kuzuia kutokea kwa ghasia kama hizo nchini humo, nchi yenye zaidi ya watumiaji milioni 18 hasa wakati wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2020.

Facebook imesisitiza kuwa tayari imefanya jitihada kubwa ili kuzuia jambo hilo lisitokee tena, lakini inahitaji kufanya jitihada zaidi.