CCM chamlilia Mwenyekiti wake Mstaafu, Mwinyi

0
179

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeeleza kupokea kwa mshtuko na huzuni kubwa taarifa za kifo cha Mwenyekiti wake Mstaafu na Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi, kilichotokea jana Februari 29, 2024.

Taarifa iliyosainiwa na Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Emmanuel Nchimbi zimesema Mzee Mwinyi atakumbukwa kwa mageuzi makubwa ya kiuchumi, kisiasa na kijami aliyoyaongoza wakati akiwa Rais wa Tanzania (1985-1995).

CCM kimesema Mwinyi pia atakumbukwa kwa jitihada zake kubwa katika kuleta madadiliko ya kiutendaji, kiuendeshaji na kimfumo ndani ya chama hicho alipokuwa Mwenyekiti wa CCM Taifa (1990-1996).

“Sambamba na hayo, daima mchango wake utakumbukwa kwa namna alivyosaidia kujenga umoja wa kitaifa na kulinda muungano, mojawapo ya tunu zetu za taifa, wakati wa utumishi wake Serikalini,” imesema taarifa ya CCM.

Chama hicho tawala kimesema kitaendelea kumwenzi Mzee Ali Hassan Mwinyi kwa yale yote mema aliyoyetendea na kuwausia Watanzania.