Halmashauri kupimwa kwa kubuni vyanzo vya mapato

0
207

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mohamed Mchengerwa amesema kigezo cha ziada cha kuzipima halmashauri zote nchini kuanzia mwaka wa fedha ujao ni kila halmashauri kubuni vyanzo vipya vya mapato kuanzia viwili na kuendelea kwa kila mwaka wa fedha.

Mchengerwa ameyasema hayo wakati wa akifungua mkutano wa 38 wa Jumuiya ya Serikali za Mitaa (ALAT) Taifa unaofanyika Zanzibar.

Amesema nguvu ya kila halmashauri ni mapato yake na ili iweze kutekeleza miradi yenye tija lazima kuwe na mapato ya uhakika.

“Hili tulishalijadili na kamati tendaji ya ALAT na kukubaliana sasa kuanzia mwaka ujao wa fedha kigezo hiki kitaingizwa rasmi katika vigezo vya upimaji wa utendaji kazi kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa,” amesema.

Aidha Mchengerwa amezitaka halmashauri zote nchini kuhakikisha zinafanya makadirio ya ukusanyaji wa mapato kwa kuzingatia takwimu sahihi za vyanzo vya mapato.