Bodi ya Barabara Mkoa wa Pwani imewaagiza Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini -Tarura kujenga haraka barabara ambazo zinafungua maeneo yote yaliyotengwa kwa ajili ya uwekezaji.
Agizo hilo limetolewa Mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Bodi hiyo Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Evarist Ndikilo wakati akifungua kikao cha bodi hiyo cha kujadili na kupitisha bajeti ya fedha zitakazitumika kujenga miradi ya barabara katika kipindi cha mwaka 2019/2020..
Pia amewataka Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini -Tarura kufungua barabara zote zinazoenda katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya uwekezaji na kutoa agizo kwa Wakala wa Barabara nchini -Tanroads pamoja na Tarura kuhakikisha barabara wanazojenga zinaendana na kiasi cha fedha kilichotengwa.
Kwa upande wake Meneja wa Wakala wa Barabara Mkoa wa Pwani, Yudas Msangi amesema katika kipindi cha mwaka 2019/2020 zaidi ya Shilingi Bilioni arobaini ma sita zimetengwa kutekeleza miradi mbalimbali ya barabara ikiwemo upanuzi wa Daraja la Mto Wami.
Naye Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini, Silvestry Koka ameishukuru serikali kwa kuanza kujenga barabara za lami katika kitovu cha mji huo.