Wapiganaji wa kikundi cha Boko Haram katika mji wa Kano nchini Nigeria wameshambulia kituo cha Polisi katika mji huo zikiwa ni siku chache tangu kikundi hicho kilipofanya mfululizo wa mashambulio mengine manne yaliyosababisha vifo vya zaidi ya watu 180.
Inasemekana Polisi katika mji huo pia wamefanikiwa kuwakamata watu kadhaa wanaotuhumiwa kuwa ni wapiganaji wa kikundi hicho cha Boko Haram katika mji huo baada ya kufanya upekuzi na habari zinasema katika oparesheni hiyo baadhi ya wapiganaji wa kikundi hicho wameuawa.
Hata hivyo watu wanaoishi katika nyumba iliyovamiwa na Polisi wamesema hawana uhusiano wowote na kikundi cha Boko Haram na Polisi wamefanya uvamizi usiokuwa halali. Kumekuwa na hali ya wasiwasi katika mitaa mbalimbali ya mji wa Kano, huku Polisi wakiendelea na doria.
