Maelfu ya watu wamekusanyika katika uwanja wa Tahrir mjini Cairo nchini Misri kuadhimisha mwaka mmoja tangu wananchi walipofanya mapinduzi ya kiraia na kumuondoa madarakani Rais wa zamani wa nchi hiyo Hosni Mubarack.
Maadhimisho hayo yanaendelea huku serikali ya kijeshi ya nchi hiyo ikiwa imeondoa sheria ya hali ya hatari iliyowekwa wakati wa utawala wa Mubarack mwaka 1967. Sheria hiyo imeondolewa leo ikiwa ni siku moja tu tangu kikao cha kwanza cha bunge la demokrasia kufanyika nchini Misri.
Sheria ya hali ya hatari nchini humo ni miongoni mwa mambo yaliyowakera raia wa Misri na kuwafanya waandamane wakimshinikiza Mubarack kuondoka madarakani.
Akitangaza kuondolewa kwa sheria hiyo kiongozi wa kijeshi nchini Misri, Hussein Tantawi amesema sheria hiyo itaendelea kutumika kupamba na vikundi vya wahuni.
Hata hivyo raia wa Misri wamekuwa na mashaka kuhusiana na sheria hiyo, hasa pale serikali ya kijeshi inaposema kuwa itatumika kupambana na vikundi vya wahuni, kwani haielezi wazi kuwa wahauni hao ni akina nani.
Kwa siku 18 waandamanaji nchini Misri walijikusanya katika Uwanja huo wa Tahrir wakimshinikiza Mubarack kuondoka madarakani. Ingawa jeshi la nchi hiyo lilijaribu kutumia nguvu kuwatawanya na kuwaondoa katika uwanja huo, waliendelea na msimamo wao hadi Mubarack akalikabidhi jeshi la nchi hiyo madaraka.
